Tuesday, December 4, 2007








Wawekezaji watawawekezea hadi surua
Na Papaa Mawani
Ni nani kasema nchi hii tuna mpango wa kuelekea kwenye U-China au U-Korea ule wa upande wa Kaskazini? Mbona hata na hawa walishashindwa na zile itikadi za kujinyima wakasarenda?
Sasa hayo ndo mwataka kuyazua tena huku Bongo? Kasema nani itatokea tena ikawa ni kazi ya ma-RC kutupangia tulime nini, tuzalishe nini au tutegemee mkakati upi wa kukabiliana na ugumu wa maisha? Mnategemea kutushika mikono na kutuelekeza tu kama vipofu bado? Hamjagundua kuwa neema tulizonkawa nazo zimekwisha?
Tukimbiliye kwenye kilimo cha nyanya au dengu siye? Mbona maeneo yenye kulipa wameshapewa wawekezaji? Mmeliwa! Naapa kwa hapa tulikofikia itafikia wakati hao wakuja wakawekeze kwenye ubuyu. Watatengeneza hadi magodoro ya sufi kama wameshaanza kuuza maua na nepi mitaani. Si kilio chetu ni kuwapata wawekezaji?
Hamjagundua kuwa kwa zama za sasa hata na Machinga wanaotembeza bidhaa mikononi wameshapata washindani? Si mwawaona maofisini na mitaani vijana wenye bidhaa nadhifu, wakiziuza kwa mtindo wa promosheni? Na bado! Uzuri wa hawa vijana wa promosheni huvaa kitanashati na tena wanajua kusalimia wateja wao; tofauti na hawa mabubu wa kikwetu. Mtashangaa sana naapa! Watakuja bado wawekezaji hadi kwenye majeneza na sanda.
Dawa za kienyeji si mwawaona Wachina wakishindana na Wamasai?
Ina maana hawa Wafipa na Wasambaa wa hapa Bongo wameshindwa kuuza dawa hadi uingie uwekezaji katika eneo hili? Tumeshapotea njia. Tunawajengea maisha bora Wachina eti? Huku kwetu ni soko mjinga eti? Kauzeni na ninyi choroko kule Uchina msipokiona cha moto. Wachina huuza tangu pikipiki, TV hadi vifaa vya umeme tena bei poa. Mshindwe wenyewe.
Wawekezaji wa sasa wananunua hadi taka. Maplastiki si yalijaa kila pahala majumbani penu? Na mitaani penu si maskrepu ya kila kitu yalizagaa? Wawekezaji wameshasikia kilio chenu na kuwekeza kwenye kuresaiko hayo maskrepu? Haya tuimbe ?Neema neema neema imefunguliwa?!
Hakuna tena chuma pahala. Kwanza ukizembea ukaacha gari kwenye gereji bubu, si kazi ukaijia na kutaarifiwa kuwa imepotea. Jamani gari kupotea? Kwa sasa yawezekana. Wawekezaji wamekuja na solusheni. Kila mtaa una kiwanda chake cha chuma chakavu. Mambo ni ujasiriamali. Kama ilifanyika upembuzi yakinifu kuhusu mahitaji au madhara ya sekta ya vyuma chakavu sielewi. Kwani ombaomba ana chaguo?. Mliwahi kumwona Matonya akichagua nipe hiki na wala siyo kile? Wataka ajira kwa wapiga kura wako au siasa?
Kila neema huja na kero yake. Hayo maviwanda sasa yameingia pabaya. Lengo lilikuwa vyuma chakavu sasa hukusanya hadi vipya. Yarabi! Halahala wasikubebee cherehani au kinu chako cha kusagisha mahindi. Hawana dini hawa.
Wameshavamia hadi vyuma vya madaraja na mabambari yaliyofungwa. Si alama za barabarani wala vibao vinavyoelekeza kwenye Taasisi mbalimbali tu bali hukumba chochote chenye sura ya chuma. Ni vijana hatari tena usiombee wakupitie kwako. Laana sasa imewafika Bongo kwa utamu wa biashara ya mavitu chakavu. Wangeishia basi huko kwenye vibao vya Cocacola, Pepri, Chibuku au safari lager.
Wamevamia hadi misalaba ya makanisa na vibao vya vituo vya Polisi. Hukusanywa kwenda kuuzwa kama skrepu. Toba! Kwa nini mnashangaa uongo kana kwamba hamkutabiri hayo kutokea? Mbona sasa ukipaki gari hovyohovyo hawatakawia kuivua rimu wakauze kama chuma chakavu? Imagini rimu ya gari inayotembea kuwa chuma chakavu. Wameacha nini kwani? Wakikuta nyaya za simu haya, za umeme ndo usiseme, ilimradi tu hazina moto.
Mifuniko ya ?inspection chambers? ndo hatupumui tena. Si majumbani si mitaani hadi mabarabarani wamekomba. Baya zaidi sasa wamevamia hata makaburini.
Ebo! Ni uwekezaji gani huu ulioandamana na laana kiasi hiki? Ujasiriamali gani huu usio na mipaka? Imagini misalaba imeandikwa RIP (Pumzika kwa Amani), lakini mtu anaishusha kama chizi. Anaipakia kwenye mkokoteni kwenda kuuza?
Wajameni, huu nao ni ujasiriamali? Mbona makaburini panahitaji heshima? Hivi wakiamka hao walolalamo wakakubamba unadokoa misalaba au vibao vya majina na diteili zao kuna mswalie mtume hapo? Ujasiriamali gani huu ambao haujatulia?
Huo ni Mkukuta au Mkakati? Hapa panatisha naapa! Si mlisikia huko Mikocheni kwenye kiwanda cha chuma chakavu yalilipuka mabomu?
Wenzetu walipata dili mabomu ya kutupa kwa mkono kwenye maeneo ya kivita na kubeba kama chuma chakavu? Viwanda vya chuma chakavu vikabadilika kuwa mstari wa mbele. Hatimaye wamevamia Reli ya Tazara bila kujali kuwa ule ni mradi wa nchi mbili tofauti na ni kifaa cha ukombozi.
Nani anayejua hayo zaidi ya Nyerere na Kaunda? Tumeliwa wima naapa! Mwadhani haramia ana uzalendo wa kujua hayo yote? Kwa mujibu wa mhishimiwa Mwakipesile wameng?oa baadhi ya reli katika Reli ya Tazara.
Mtume! Mbona hili ni hatari kuliko lile la kuiba mafuta ya transfoma za Tanesco, kwa ajili ya ukaangaji chipsi au kutengeneza losheni? Ufisadi kuliko huu ni upi? Mwakipesile lilimwuuma sana hili kama Mkuu wa Mkoa na kada wa Chama Tawala.
Kwa paniki ilompata alinyanyua maiki na kukemea kuwa sasa hawa watu wameelekea pabaya. Aliwataka hawa wajasiriamali wa chuma chakavu wakome na wakomae. Alisisitiza kuwa hataruhusu yeyote mkoani mwake kushughulika na ujasiriamali wa chuma chakavu. Bahati mbaya kila kitu wanaita chuma chakavu hata wangekuwa wasomi. Kwa hapa hawakushughulikia chuma chakavu.
Reli ni chuma mpya na siyo chakavu. Hivi Mwakipesile alikuwa serious?? Akikemea biashara hiyo mkoani Mbeya ina maana amewazuia kuifumua reli hiyo? Kwani hawawezi kuendelea kuifumua reli ya Tazara wabebe vyuma hivyo na kuviuza mkoani Iringa au Ruvuma? Kwa hiyo amewaruhusu hao wajasiriamali wakauzie mikoa jirani siyo?
Mwakipesile kama mwakilishi wa Rais na mlinzi wa maslahi ya Taifa anaishia mkoani pake tu? Hivi Mwakipesile atueleze kama uzalendo una mipaka. Mbona alipaswa kuwashauri Waziri wa Miundombinu na yule wa Biashara/Viwanda wapange mkakati wa kukabiliana na zahama hii? Badala yake anaishia Mwanjelwa na Ipogoro tu? Huu ni mzaha naapa! Mwisho




  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.comme google-site-verification=Qm-XNfnL5kai8WV2inT1RRX2WIPaBTG_WPq3kYSBwbgKennedy Kimaro 2008 NYUMBANI NI NYUMBANI TU KUMBUKA KUWEKEZA NYUMBANI LEO

Rudi TOP-Juu