Friday, November 30, 2007

Ukaguzi wa Benki Kuu Tanzania wabaini kasoro














Ukaguzi wa Benki Kuu Tanzania wabaini kasoro

*Ripoti za awali zaonyesha utata
*Baadhi ya vigogo BoT watajwa kuhusika
*Wahusika kuchukuliwa hatua
*Meghji asema hajaipata, iko kwa CAG
Na Ramadhan Semtawa
JOTO la tuhuma za ufisadi katika Akaunti ya Madeni ya Nje katika Benki Kuu ya Tanzania (BoT) limepanda, kutokana na taarifa za awali za ukaguzi kuonyesha kuwa kuna utata katika matumizi ya akaunti hiyo.
Ukaguzi huo ulifanywa na Kampuni ya Ernst & Young katika kipindi cha siku 60, kuanzia Septemba na kukabidhi ripoti yake kwa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG) wiki iliyopita.
Hata hivyo, ikiwa ni wiki moja tangu CAG kukabidhiwa ripoti hiyo, taarifa za awali kutoka vyanzo mbalimbali vya habari ndani na nje ya serikali, zinaeleza kwamba baadhi ya vigogo ndani ya BoT wanatajwa kuhusika na malipo hayo yenye utata.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, vigogo hao wanahusishwa na ama kuidhinisha au kuhusika kwa namna moja au nyingine katika malipo hayo.
Vyanzo hivyo vilifafanua kwamba, maamuzi kuhusu ripoti hiyo yanatarajiwa kuchukuliwa kabla ya mwaka mpya.
"Watu watapata zawadi ya mwaka mpya, uchambuzi unaendelea kufanyika, lakini taarifa za awali zinaonyesha hivyo," kilisema chanzo cha habari kutoka serikalini.
Vyanzo hivyo vilifafanua kwamba, kuna baadhi ya stakabadhi za malipo ambazo zimeanza kuchambuliwa na zinaonyesha kuwa zimejaa utata.
Kwa mujibu wa taarifa hizo, uchambuzi huo umezingatia kwa kina nyaraka za msingi za malipo ili kuona utata huo unasababishwa na nini.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo, ukaguzi huo ambao uliingia kwa ndani na kuhoji watu mbalimbali akiwemo Waziri wa Fedha, Zakia Meghji unaweza kubadili hali ya kisiasa nchini katika kipindi cha kuingia mwaka mpya wa 2007/08.
Meghji alipoulizwa ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana kuhusu ripoti hiyo, alisema hadi sasa bado iko kwa CAG.
Alisema hafahamu lolote kuhusu kilichomo ndani ya ripoti hiyo kwani hajaiona na wala hawezi kuzungumza yaliyomo kwa sasa.
"Hadi sasa ripoti iko kwa CAG, sijaipata kama ni suala la maamuzi na nini kilichomo ni hadi ichambuliwe, nikiipata, nitaipitia, atapewa Rais na maamuzi yatatangazwa kwa umma," alisema Meghji.
Kauli hiyo ya Meghji ni ya pili ambapo ya kwanza ilitolewa na CAG ambaye wiki iliyopita alisema ofisi yake inafanyia kazi mambo yaliyomo katika ripoti hiyo, lakini hakufafanua.
Ernst & Young, awali ilipaswa kuikabidhi ripoti yake serikalini Novemba 10 ikiwa ni kumalizika kwa siku 60 za kufanya ukaguzi huo, lakini haikufanya hivyo na kuiomba serikali wiki tatu kwa ajili ya kuandaa ripoti ambayo ilifanyikia London, Uingereza.
Ripoti hiyo inasubiriwa kwa hamu na Watanzania kuona ukweli wa tuhuma za ufisadi ambazo zinadaiwa kufanywa katika EPA kwa ajili ya malipo ya vocha mbalimbali.
Nchi wafadhili pia zimesema zinasubiri kwa hamu matokeo ya uchunguzi huo kwani ni kipimo cha kuona mwelekeo wao wa kuongeza misaada kwa Tanzania katika bajeti ya mwaka 2008/09.
Kampuni hiyo ilipitia mahesabu katika kumbukumbu za vocha za malipo yaliyofanywa na BoT katika kipindi cha mwaka 2005/6, kubaini kama kuna ukweli juu ya madai ya ubadhirifu wa fedha katika benki hiyo katika kipindi hicho.
Agizo la kutafuta kampuni ya kukagua vocha hizo na mahesabu ya BoT, lilitolewa na Waziri Meghji Desemba 3, mwaka jana akimtaka CAG kuteua kampuni huru ya wakaguzi wazoefu wenye sifa za kimataifa kupitia baadhi ya kumbukumbu za matumizi ya fedha za benki za mwaka 2005/2006 ili kuondoa utata.







Makala
Habari nyingine zaidi!
Alia kwa watoto wake wawili walemavu kukosa masomo



INGAWA elimu ni haki ya mtoto na msingi kwa kila mtoto, Asia Kawi na mdogo wake anaitwa Ahmed, wamekosa nafasi ya kujiunga na shule kutokana na hali yao ya ulemavu,” anasimulia mama yao Mwanahawa Juma. Mwanahawa anasema watoto wake wamekosa nafasi ya kujiunga na shule ya viziwi, jambo linalosababisha wakose elimu ambayo ingewasaidia maishani. Watoto hao wenye uchu wa elimu huamka saa 11.30 alfajiri na kuvaa sare za shule kisha kukaa sebuleni huku wakinyoosha vidole kuelekea mlango ili kuashiria kuwa wanataka kutoka nje. Wanapofunguliwa milango, watoto hukaa barazani na kuwapungia watoto wenzao wanaopita eneo hilo kuelekea shuleni. Watoto hao wanaozungumza kwa lugha ya ishara kila mara wanamsihi mama yao awapeleke shule. “Jambo hili huwa linaniumiza na ni pigo kubwa kwa watoto wangu….walizaliwa wakiwa wazima kisha wakaugua na kuteseka kipindi chote cha utoto wao…na sasa wanaendelea kuteseka kwa kukosa nafasi ya masomo,” Mwanahawa anaeleza akiwa anabubujikwa na machozi. Hivi sasa Asia ana miaka 15 lakini ameshindwa kupata elimu sahihi kulingana na ulemavu wake, kwani mama yake amejitahidi kumtafutia shule ya elimu maalumu kwa viziwi bila mafanikio. Mwanahawa anasema mtoto huyo alipotimiza umri wa kwenda shule alimpeleka katika Shule ya Msingi Viziwi Buguruni lakini hakufanikiwa kupata nafasi ya masomo. “Nilikwenda kumwandikisha katika shule ya msingi Viziwi Buguruni akajumuishwa na watoto wengine kwa ajili ya usaili na baadaye uongozi wa shule ulinijulisha kuwa amekosa nafasi,” Mwanahawa anasema kwa huzuni. Baada ya kubaini kuwa mtoto wake amekosa nafasi katika shule ya elimu maalumu kwa viziwi, aliamua kwenda kumuandikisha katika shule ya Msingi Uhuru Mchanganyiko. Mwanahawa alikuwa akimpeleka mwanawe shuleni kila siku kwa kipindi cha miaka minne, lakini mtoto huyo hakuwa anaelewa kitu kwa sababu hakuwa anafundishwa kwa lugha ya ishara. “Asia alichanganywa na watoto wenye taahira ya akili na mtindio wa ubongo na kuhudhuria masomo kwa miaka minne lakini alikuwa haelewi kitu chochote, hata hivyo nilibaini kuwa akifundishwa kwa lugha ya ishara anaelewa,” Mwanahawa anaeleza. Baada ya kubaini kuwa mtoto huyo anahitaji elimu maalumu kwa watoto viziwi, aliamua kutoendelea kumpeleka shule ya Uhuru Mchanganyiko kutokana na ukweli kuwa alikuwa akitembea umbali mrefu kwenda kufuata huduma ambayo haipo. Anasema alirudi tena katika shule ya viziwi Buguruni kuomba nafasi kwa ajili ya Asia lakini hakufanikiwa, jambo linalosababisha mtoto huyo kukaa nyumbani. “Ahmed alipofikisha umri wa kwenda shule nilikwenda tena katika shule ya Msingi Viziwi Buguruni kuomba nafasi…walimwita kufanya usaili kisha wananiambia kuwa hakuna nafasi kwa kuwa shule hiyo inachukua wanafunzi wachache,” Mwanahawa anaeleza. Anadai kuwa ameomba nafasi hiyo kwa miaka minne mfululizo lakini hakufanikiwa, jambo linalosababisha watoto wote wawili kukaa nyumbani baada ya kukosa nafasi katika shule ya elimu maalumu kwa viziwi. Anadai baada ya kwenda katika shule hiyo mara kwa mara walimshauri ampeleke Ahmed katika shule ya Msingi Mugabe ambako kuna kitengo cha elimu maalumu kwa watoto wenye ulemavu wa kusikia na kuzungumza. Hata hivyo, Mwanahawa anasema ameshindwa kumpeleka mtoto huyo katika shule iliyopo Sinza kwa kuwa kuu mbili. Kwanza hana kipato kitakachomwezesha kugharamia nauli ya kumpeleka shule kila siku, pili ana mtoto mwingine mlemavu ambaye naye anahitaji uangalizi maalumu. “Nimetamani sana watoto wangu wasome Buguruni kwa sababu ni kama dakika saba tu kufika shuleni…ninaweza kuwashika mkono na kuwapeleka…nasikitika kwa kuwa shule ya msingi Buguruni Viziwi haipo mbali na ninakoishi, lakini watoto wangu hawakupata bahati ya kuifaidi,” Mwanahawa anasema kwa huzuni. Anaendelea kusema, “wakati mwingine nahisi kuwa umasikini wangu ndio unaosababisha watoto wangu wakose nafasi ya masomo. Kama ningekuwa na uwezo wa kifedha au cheo fulani wanangu wangepewa kipaumbele kwa kuwa ni wakazi wa Buguruni, lakini wote wawili wamekosa shule…nasikitika sana.” Mwanamke huyo mjane, asiyekuwa na uhakika kwa kupata mlo wa siku anawaomba wasamaria wema na taasisi mbalimbali zijitokeze na kusaidia kugharamia masomo ya watoto wake ili waweze kupata elimu itakayowasaidia maishani. “Bila elimu watoto hao hawataweza kushiriki vyema katika shughuli za maendeleo ya kiuchumi na kijamii na badala yake watakuwa mzigo…wataishi katika hali ya ufukara kwa sababu mimi mwenyewe sina uwezo wa kuwajengea msingi imara kwa maisha yao ya baadaye,” anaeleza. Katibu wa Chama cha Viziwi Tanzania, Matilda Ngonyani anasema uongozi wa shule hiyo utakuwa mstari wa mbele kujiunga na taasisi na wasamaria wema watakaojitokeza kutoa msaada kwa watoto hao. “Tumepokea kwa mshtuko taarifa kuhusu watoto hao…sisi tutawasaidia kwa kuwa kila mtoto ana haki ya kusoma kulingana na mahitaji ya ubongo wake…ikiwa kweli watafaa katika darasa la viziwi tutawapokea ingawa nafasi ni finyu,” anaema Ngonyani. Anafahamisha kuwa shule hiyo inayosimamiwa na Chama cha Viziwi Tanzania, haibagui watoto viziwi lakini inakabiliwa na changamoto kubwa kwa sababu haiwezi kuchukua wanafunzi zaidi ya 30 kwa mwaka. “Kila mwaka tunachukua wanafunzi 20 kwa darasa la kwanza na 10 wa shule ya awali…wanafunzi hao wanatoka sehemu mbalimbali nchini na tunawagharamia kila kitu…wazazi wao hawalipii chochote,” Ngonyani anasema. Hata hivyo, anasema ufinyu wa nafasi katika shule hiyo siyo sababu ya kutowapatia Asia na Ahmed nafasi ya kusoma katika shule hiyo na ameahidi kufuatilia ili kubaini tatizo. “Huenda walikosa nafasi kwa sababu wana tatizo zaidi ya moja, mfano taahiri ya akili na mtindio wa ubongo, kutokuona au ulemavu mwingine ambao unasababisha wasiendane na kundi la viziwi,” Ngonyani anaeleza. Ngonyani, ambaye ni mmoja wa wajumbe wa bodi inayomiliki shule hiyo, anaeleza kuwa shule hiyo inafanya uchunguzi wa kina kuhakikisha wanaopata nafasi katika shule hiyo ni kundi la viziwi pekee ili kuepuka vikwazo vinavyosababishwa na watoto wenye ulemavu zaidi ya mmoja. “Mfano tukichukua mtoto mwenye ulemavu wa taahira ya akili na mtindio wa ubongo au mwenye otizim atakuwa anafanya mambo tofauti na wenzake hivyo watoto wengine wataacha kuzingatia masomo na kuanza kudadisi mwenendo wa mwenzao anayefanya mambo tofauti…, jambo hilo linatufanya tuwe makini sana wakati wa kuchukua wanafunzi viziwi,” Ngonyani anaeleza. Anafafanua baadhi ya watoto wenye taahira ya akili na mtindio wa ubongo au wenye otizim wana tabia ya kukaa kimya au kukaidi wanapoitwa, jambo linalosababisha wazazi waamini kuwa wana ulemavu unaosababisha washindwe kusikia na kuzungumza. Ili kubaini tatizo hilo watoto wanaopelekwa katika shule hiyo hufanyiwa uchunguzi wa masikio ili kupima uwezo wao wa kusikia. Pia hufanyiwa majaribio mengine kama vile kuchagua rangi, kupanga vitu mbalimbali kwa kufuata ukubwa na kuchora mstari. Kwa kuwa watoto hao ni wadogo tunawapa majaribio mepesi ili kutambua matatizo yao. Mfano wataalamu wanapanga herufi au maumbo yenye rangi mbalimbali ambapo mtoto anapaswa kuigizia akichagua herufi tofauti au rangi tofauti na wataalamu wanatambua ana matatizo ya macho au tatizo jingine mbali na kutosikia. “Unaweza kuchora mstari na kumuambia mtoto achore anachokiona…badala ya kuchora mstari anaandika nukta nukta au anaambiwa aweke maumbo kwenye mashimo kulingana na ukubwa anachukua umbo kubwa analazimisha liingie kwenye shimo dogo….hapo wataalamu wanabaini kuwa watoto hawa sio viziwi ila wana matatizo ya ubongo ambayo yanawakosesha mawasiliano,” Ngonyani anafafanua. Hata hivyo, anasisitiza hivi sasa Tanzania ina vitengo mbalimbali vya elimu maalumu wa watoto wenye ulemavu hivyo Asia na Ahmed hawana sababu ya kukosa elimu. “Kwa kuwa hakuna binadamu aliye kamili inawezekana hata sisi tulipitiwa…tumelichukulia suala hilo kwa uzito mkubwa …ikiwa ni viziwi tutawapatia nafasi…Asia anaweza kujiunga na shule ya ufundi na Ahmed akaingia shule ya msingi…hata wakiwa na tatizo lingine tutamshauri mama yao na kumwelekeza pa kuwapeleka,” Ngonyani anasema. Mwalimu Mkuu wa Shule ya Msingi Viziwi Buguruni, Said Mkude anasema, anaomba Serikali iangalie uwezekano wa kuongeza vitengo vya elimu maalumu kwa watoto wenye ulemavu ili kuhakikisha kuwa kila mtoto anapata haki ya kusoma. Mkude anafahamisha kuwa amewasilisha maombi yake kwa Ofisa Elimu wilaya ya Ilala na kumfahamisha kuwa ipo haja ya kuongeza vitengo vya watoto viziwi katika shule za kawaida kwa kuwa shule yake haiwezi kuchukua watoto wote wanaomba nafasi za masomo. Akitoa mfano Mkude anasema kwa mwaka huu, watoto 78 waliombewa nafasi ya kujiunga na darasa la kwanza, kati yao wavulana 47 na wasichana 31. Waliohudhuria usaili ni 53 kati yao wavulala 33 na wasichana 20. “Kati ya wavulana 33 waliochaguliwa ni 9 na kati ya wasichana 20 waliochaguliwa ni 11 hivyo kukamilisha idadi ya wanafunzi 20 wa darasa la kwanza lenye michipuo miwili….pia tumechukua wavulana sita na wasichana wanne wa darasa la awali. Hivyo watoto zaidi ya 23 waliofanya usaili wamekosa nafasi,” Mkude anaeleza. Anaendelea kusema,"Tukijumlisha na watoto ambao hawakufika kwenye usaili ni dhahiri kuwa wastani wa watoto viziwi 45 wanakosa nafasi za masomo baada ya wazazi wao kuonyesha nia ya kuwasomesa……hivyo Serikali na wadau wa elimu wanapaswa kulipa uzito jambo hili na kulitafutia ufumbuzi ili watoto wenye ulemavu waweze kupata elimu.” Ikiwa Serikali ina dhamira ya kweli ya kuhakikisha kuwa watoto wote wenye umri wa kwenda shule wanasoma, inapaswa kufuata ushauri uliotolewa na shule vya Viziwi Bunguruni na kuongeza vitengo vya elimu maalum kwa watoto wenye ulemavu nchini. Wanaotaka kuwasaidia Asia na Ahmed wawasiliane na mama yao kwa simu namba 0754 364 085.

Thursday, November 29, 2007

Je studio gani ni ya mwaka 47 na ipi ni ya kisasa ?

Studio ilivyo kituo cha tv ITV TanzaniaStudio ilivyo katika kituo cha Tv NATION Kenya

Ingekuwa katika kipindi cha Redio one kinachojulikana kwa nani zaidi
Wewe mdau ungekuwa upande gani? na kwa nini!
je ni studio ipi! ni ya mwaka 47? na ipi ni ya Kisasa!

Wabunge Canada wahoji ziara ya Waziri Mkuu wao nchini Tanzania

Hakuna kama Nyerere mpaka sasa
Miaka 46 ya Uhuru








Wabunge Canada wahoji ziara ya Waziri Mkuu wao nchini Tanzania



Na Mwandishi Wetu
ZIARA ya Waziri Mkuu wa Canada Stephen Harper nchini, imeibua mambo mapya, baada ya baadhi ya wabunge na viongozi wa serikali ya nchi yake, kupinga kukutana na uongozi wa Kampuni ya Madini ya Barrick katika kikao cha faragha.
Kabla ya kumaliza ziara yake, Harper alikuwa na kikao cha siri kilichoandaliwa na Ubalozi wa Canada nchini na kudumu kwa dakika 45, kuzungumza na makampuni ya Canada ikiwemo ya Barrick.
Paul Dewar, Mbunge wa Jimbo la Ottawa ya Kati (NDP), alisema Harper alipaswa kukutana na watu walioathirika na uamuzi wa kampuni hiyo kuwafukuza kazi baadhi ya wafanyakazi wake na kujua hatma yao.
�Kampuni ya Barrick imesababisha mtafaruku kwenye jamii ya Watanzania, Waziri Mkuu alitakiwa akutane moja kwa moja na watu walioathirika na maamuzi ya Barrick kuwafukuza wafanyakazi wake wasio na chombo cha kuwatetea badala ya kukutana na uongozi wa kampuni,� alisema Dewar ambaye pia ni Waziri Kivuli wa Mambo ya Nje, katika mahojiano na Gazeti la Toronto Star juzi. na kuongeza;
� Alipaswa kuangalia mazingira halisi ya kampuni hii kushindwa kujali usalama wa wafanyakazi hao.�
Vilevile, Joan Kuyek Mratibu wa Kitaifa wa Kikundi kinachofuatialia taratibu za uchimbaji madini kwenye migodi cha MiningWatch, alisema kitendo cha Kampuni ya Barrack kutojali maslahi ya wafanyakazi wake katika nchi za Chile na Tanzania, kinakiuka taratibu za kimataifa za uchimbaji madini.
Alisema nchini Chile, Kampuni hiyo imekuwa ikilalamikiwa kwa uharibifu wa mazingira na kutojali usalama wa wafanyakazi wake, mambo ambayo pia yamekuwa yakilalamikiwa Tanzania.
�Kama Waziri Mkuu Harper amekutana na wawakilishi kutoka Barrick pekee na hakukutana na wachimbaji wadogo, wala watu wanaoshughulikia athari za kijamii, kiuchumi na kimazingira kwenye maeneo ya migodi nchini Tanzania, wala wawakilishi wao, hii inashtua sana! � alisema Kuyek.

Kamati ya madini yageuka kama maigizo

*Mwingine aandika barua ya kujitoa
*Aliyejitoa wa kwanza, wa pili wahudhuria
* Iddi Simba ahamaki waandishi kuwako ndani
* Bomani awataka wajumbe kuweka maslahi ya taifa mbele

Muhibu Said na Mwanaid Omary
KAMATI ya Kuangalia Upya Mikataba ya Uchimbaji Madini nchini, imeanza rasmi kazi zake jana, huku wajumbe wake wawili walioomba kwa Rais Jakaya Kikwete kujitoa , wakishiriki.
Wajumbe hao, ni Peter Machunde kutoka Soko la Hisa la Dar es Salaam (DSE) na Mkaguzi wa Mahesabu kutoka Kampuni ya Kimataifa ya Ukaguzi wa Mahesabu ya PriceWaterhouse Coopers, David Tarimo.
Hata hivyo, wakati hayo yakijiri, katika moja ya kazi zake, kamati hiyo imepanga kukutana na wenyeviti wa kamati zilizoteuliwa katika siku za nyuma kuchunguza kuhusu madini ili kupata uzoefu wao katika suala hilo, kuanzia Jumatatu na Jumanne wiki ijayo.
Kamati hizo, ni ile ya Jenerali Robert Mboma iliyoundwa mwaka 2001, ya Brigedia Mang'enya ( 2003), ya Dk Kipokola (2004) na ya Masha (2006).
Machunde alitangaza kujiuzulu wiki iliyopita kwa madai ya kukerwa na maneno ya baadhi ya viongozi wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ya kumtaka ajitoe katika kamati hiyo kwa madai ya kuwa na urafiki wa karibu na mmoja wa mawaziri wa serikali ya awamu ya nne.
Taarifa za Tarimo kuomba kujitoa , zilitangazwa jana na Mwenyekiti wa Kamati hiyo , Jaji Mark Bomani wakati akifungua kikao chao cha kwanza katika Ofisi za Bunge, jijini Dar es Salaam.
Akitoa taarifa hiyo, Jaji Bomani, alisema Tarimo aliwasilisha barua ya kujitoa katika kamati hiyo kama mjumbe kwa madai kwamba kampuni yake inatumiwa na baadhi ya makampuni ya madini, hivyo, ana wasiwasi ushiriki wake unaweza kuleta mgongano wa maslahi, lakini alisisitiza kuwa, atakuwa tayari kutoa ushauri utakapohitajika.
Hata hivyo, Jaji Bomani alishindwa kusoma barua ya Tarimo, baada ya mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo, Iddi Simba kumzuia asifanye hivyo mbele ya waandishi wa habari kwa madai kwamba, iwapo jambo hilo litawafikia wananchi, linaweza kuibua malumbano mitaani.
" Watupishe kwanza waandishi wa habari, tujadili sisi wenyewe, pengine baadhi yetu tunataka (Tarimo) asijitoe," alisema Iddi Simba na kuungwa mkono na Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige.
Kutokana na ushauri huo, Jaji Bomani aliwataka waandishi wa habari wasitangaze habari hizo kwa muda huo na badala yake wasubiri hadi kamati imalize majadiliano kuhusiana na jambo hilo, kisha mchana watapewa taarifa.
Maelekezo hayo ya Jaji Bomani, yalipingwa na Mbunge wa Kigoma Kaskazini (Chadema), Zitto Kabwe, aliyesema kuwa, haoni ni busara kuwaita waandishi wa habari kila baada ya kikao na kuishauri kamati iwaruhusu wakaripoti yale waliyokwishayapata kwa muda ule.
Mapema, Tarimo alikataa kuzungumza chochote alipoulizwa na Jaji Bomani kama ana jambo la kuzungumza kuhusiana na hilo na kumuomba mwenyewe (Bomani) azungumze badala yake.
Awali, akieleza sababu za kuendelea kushiriki kwenye kamati, Machunde alikiambia kikao cha kamati kuwa, amelazimika kufanya hivyo kwa kuwa hadi kufikia jana alikuwa hajapokea majibu kutoka kwa Rais Jakaya Kikwete ya kuomba kujitoa katika kamati hiyo.
" Mpaka sasa sijapata jibu la ombi langu kwa Rais. Hivyo, nitakuwa mkosefu wa heshima kama sitashiriki katika vikao vya kamati kabla sijapata jibu kutoka kwa Rais," alisema Machunde.
Baadaye mchana, Jaji Bomani alikutana na waandishi wa habari na kuwaeleza kuwa, wajumbe walioomba kujitoa kwenye kamati hiyo, walishiriki kikao cha jana na kuongeza kuwa ana matumaini kuwa wataendelea kushiriki.
Hata hivyo, tofauti na alivyosema awali, alikanusha Tarimo kuwasilisha barua ya kuomba kujitoa, bali barua hiyo inahusu wasiwasi wa kushiriki kwake kwenye kamati.
" Tunatumai wasiwasi hautakuwapo, atafanya kazi vizuri na hakutakuwa na mgongano wa maslahi, " alisema.
Kuhusu wajumbe wengine waliotakiwa na Chadema kujitoa kwenye kamati hiyo kutokana na kutuhumiwa kwa ufisadi au mgongano wa maslahi, alisema katika kikao cha jana, hakukuwapo na majadiliano kuhusu wajumbe wengine zaidi ya Mchunde na Tarimo.
Jaji Bomani, alisema kikao cha jana ambacho kilihudhuriwa na wajumbe wake wote, isipokuwa wawili kutokana na kupatwa na udhuru, kili panga ratiba na kuafikiana namna kamati itakavyotekeleza majukumu yake.
Alisema mbali na kukutana na wenyeviti au wawakilishi wa kamati zilizoteuliwa katika siku za nyuma kuchunguza kuhusu madini, pia watakutana na wadau mbalimbali pamoja na umoja wa wachimbaji madini na kutembelea kwenye maeneo yenye shughuli za machimbo.
Jaji Bomani , alisema katika ratiba hiyo, pia watembelea nchi zenye sekta ya madini ili kujifunza namna wanavyoedesha shughuli za madini na kutoa nafasi kwa wananchi kutoa maoni kabla ya kamati kukaa na kutafakari waliyoyapata na kuandaa ripoti watakayoiwasilisha serikalini katika muda muafaka.
Hata hivyo, alisema kutokana na muda na gharama kuwa finyu, watachagua nchi chache ambazo zimepata mafanikio katika shughuli za madini na kwamba, hadi kufikia jana walikuwa bado hawajakamilisha orodha ya nchi hizo na tarehe ya kuanza ziara hiyo.
Awali, akifungua kikao hicho, Jaji Bomani aliwapongeza wajumbe kwa kuteuliwa kwenye kamati, lakini akawapa pole kwa maelezo kwamba, jukumu walilopewa ni nyeti na zito.
Hata hivyo, alisema watafanya kazi kwa bidii, uaminifu wa hali ya juu ili mapendekezo yatakayotolewa na kamati yawe na maslahi mazito kwa taifa.
Aliwataka wajumbe wawe huru kutoa maoni yao wenyewe, na siyo ya kutumwa na chombo au taasisi au chama, kwani wameteuliwa kwa sifa binafsi.
" Tutoe fikra zetu na mependekezo yetu, tusiwe na ubinafsi, tutapelekea kupishana katika kutoa mapendekezo ya kamati. Tutoe mapendekezo ya kamati ili kazi yetu ifanyike kwa uwazi, siyo kwa siri siri. Pia katika ratiba yetu tutoe nafasi watu watoe mawazo yao hadharani na wakaribishwe wasomi watoe mawazo yao ili yafanyiwe kazi, " alisema Jaji Bomani.
Alisema kabla ya kutangaza mapendekezo yao, watashauriana na Rais Kikwete kwamba, wayatangaze au wampe ayapitie kwanza.
Akizungumza katika ufunguzi huo, Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), John Cheyo, alisema kazi iliyo mbele yao ni nzito, hivyo, akawataka Watanzania wawaombee kwa Mwenyezi Mungu wapate hekima ya kutoa maamuzi mazuri kwa kuwa, nia yao ni moja ya kujaribu kusaidia taifa kupata maslahi kutokana na utajiri wa madini uliopo nchini.
Wajumbe wengine wa kamati hiyo ni Mwanasheria wa Wizara ya Nishati na Madini, Salome Makange, Kamishina wa Sera Wizara ya Fedha, Mugisha Kamugisha, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Makazi Wizara ya Ardhi, Edward Kihundwa, Mbunge wa Kyela (CCM), Dk Harrison Mwakyembe na mtaalamu wa masuala ya kodi na Mkurugenzi wa Madai na Sheria za Kimataifa, Wizara ya Katiba na Sheria, Maria Kejo.
Kamati hiyo iliundwa na Rais Kikwete Novemba 13, mwaka huu na itatekeleza kazi yake kwa kipindi cha miezi mitatu ambayo ni pamoja na kuchambua mfumo wa kodi unaotumika katika sekta ya madini na kupitia mfumo wa usimamizi wa shughuli za uchimbaji mkubwa unaofanywa na serikali.
Mengine ni kukutana na taasisi zinazosimamia madini na wadau wengine na kutakiwa kutoa taarifa yenye mapendekezo na kupitia mikataba ya madini na nyaraka nyingine zitakazohusu migodi ya mikubwa nchini.


Wednesday, November 28, 2007

Unamkumbuka Profesa Ndumilakuwili na Msemo wake Hakuna kulala

Click picha kupata kubwa Kitabu hiki cha Profesa kilitungwa na ndugu Karim Swago, kama nakala bado hipo pata yako
Kwani ni Moto kweli kweli ...../Hapa ni kumbukumbu ya vijitabu vya katuni zenye mvuto kwa wengi wetu, si unakumbuka Sani kina kipepe. Pimbi. bob Mazishi kina Zena na wengi tu


Dereva amlipua risasi mwenzake wakigombea abiria


Dereva amlipua risasi mwenzake wakigombea abiria
Na Daniel Mjema, Moshi

MFANYABIASHARA wa mabasi yanayofanya safari kati ya Moshi na Kilema, anashikiliwa na polisi kwa tuhuma za kumpiga risasi, dereva wa basi la Flora Coach kwa madai ya ugomvi wa kugombea abiria.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Lucas Ng'hoboko jana aliliambia Mwananchi kuwa, mfanyabiashara huyo ametiwa mbaroni tangu amjeruhi kwa kumpifa risasi mguuni dereva huyo, Rodgers Lyimo, jumamosi iliyopita.
Tukio hilo lilitokea majira ya saa 11: 30 jioni katika maeneo ya Kilema Wilaya ya Moshi Vijijini baada ya basi la mfanyabiashara huyo na lile linaloendeshwa Rodgers aina ya Toyota DCM kufika mwisho wa safari.
" Ni kweli tunaye huyo mfanyabiashara tangu Jumamosi, walizozana na huyo dereva basi
akaamua kuchukua bastola yake na kumpiga risasi ya mguu�tunaendelea kumhoji, " alisema Ng'hoboko.
Akizungumza na Mwananchi kwa simu kutoka katika Hospitali ya Kilema alikolazwa kwa matibabu, Rodgers alidai kuwa, chanzo cha tukio hilo ni kitendo cha abiria kuteremka kwenye basi la mfanyabiashara huyo na kuingia katika basi analoendesha.
Dereva huyo alidai kuwa, Ijumaa iliyopita majira ya 10:30 jioni, wakiwa katika stendi kuu ya mabasi Moshi, abiria waliingia katika basi lake na kuliacha lile la mfanyabiashara ambalo lilikuwa limepanga foleni mbele yake.
Alisema malalamiko yao, yalifikishwa kwa Meneja wa kituo hicho na kuwasuluhisha kwa
kumuagiza dereva huyo kuwasihi abiria watelemke na kupanda kwenye basi lililokuwa mbele.
" Abiria waliteremka lakini wengi hawakwenda kupanda hilo basi wakasubiri la kwangu
kwa hiyo tukajikuta tumepata abiria mapema na kumpita njiani akiwa bado anatafuta
abiria kitendo ambacho naamini hakikumfurahisha, " alidai.
Dereva huyo, alidai Jumamosi baada ya kumaliza safar,i alimkuta mfanyabiashara huyo katika baa moja iliyopo Kilema na kumsalimia, lakini alikataa kuitikia, akisema alikuwa akimtafuta kwa siku nyingi.
Alidai baadae mfanyabiashara huyo, alimfuata na kumnyang'anya kofia kisha kumpiga
dereva huyo kwa ubao mgongoni na kuanguka na kwamba wakati akiwa katika harakati za kujitetea alimsukuma mfanyabiashara huyo na kuanguka.
"Niliamua kuondoka na kurudi mahali nilipoegesha basi, lakini akanifuata na kuchomoa bastola huku akisema lazima anivunje mguu ili nisimkoroge tena katika kupakia
abiria, "alidai.
Dereva huyo aliongeza kuwa, baada ya kuchomoa bastola, baadhi ya wananchi waliojitokeza kuamua ugomvi lakini walikimbia ndipo mfanyabiashara huyo alimpiga risasi na kutiwa mbaroni baada ya tukio hilo kuripotiwa polisi.

Tuesday, November 27, 2007

Pata channel via dish lako


Kwa wale wote wanaotumia Dish kupokea local chanel na wanapata channel ya etv
Basi mwambie fundi wako akuwekee frq hii 12522 symbol rate 26657 na utapata channel ya
French English keep enjoy na Dish lako

Waziri Mkuu Canada umechelewa kuja Tanzania (Mhariri)




Waziri Mkuu Canada umechelewa kuja Tanzania (Mhariri)



Monday, November 26, 2007

Sakata la upasuaji tata-MOI: Je taratibu hazikufuatwa?



Sakata la upasuaji tata-MOI: Je taratibu hazikufuatwa?
Na Mwasu Sware na Jackson Odoyo.
WASWAHILI husema haraka haraka haina baraka, na mwenda pole hajikwai methali zote zina maana ya kuwa endapo mtu atafanya jambo kwa haraka bila kuzingatia, matokeo yake huwa ni mabaya, na ukifanya jambo kwa uangalifu matokeo yake huwa ni mazuri.
Hivi karibuni kumetokea jambo la kusikitisha ikiwa pia ni la kutatanisha juu ya kuwepo kwa upasuaji tata uliotokea katika Taasisi ya Mifupa (MOI), kwenye Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Upasuaji huo ambao uliwahusisha vijana wawili ambao ni Emmanuel Mgaya (19) ambaye alikuwa ana tatizo la kichwa lakini badala yake akafanyiwa upasuaji wa mguu, na yule Emmanuel Didas (20), aliyekuwa na tatizo la mguu alifanyiwa upasuaji wa kichwa.
Kutokana na tukio hilo baadhi ya watu hususan ndugu wa wagonjwa hao wameonekana kusikitishwa, kushangazwa na tukio hilo kiasi kwamba jamii imekuwa na woga dhidi ya huduma ya upasuaji inayotolewa katika Taasisi hiyo.
Akizungumzia tukio hilo lilivyokuwa kwa mtoto wake, mama mzazi wa Emmanuel Mgaya, Mary Mgina anasema, alifika hospitalini hapo akitokea Njombe mkoani Iringa wiki mbili zilizopita kwa lengo la mtoto wake kuja kupatiwa matibabu ya kichwa ambayo yamekuwa yakimsumbua muda mrefu.
�Tumekuja wiki mbili zilizopita tukitokea Njombe katika hospitali ya kibena ambapo tuliandikiwa barua ya kuja huku Dar es Salaam kwa ajili ya matibabu zaidi, mwanangu ameanza kuumwa na kichwa mara baada ya kuanza mtihani wa kidato cha nne akiwa ndani ya chumba cha mitihani shuleni kwake,� anasema mama yake.
Naye mjomba wa Mgaya, Dick Mgina anasema, siku ya kufanyiwa upasuaji mgonjwa wao alichukuliwa kutoka kwenye wodi ya Sewahaji chumba namba 17, na kisha kupelekwa kwenye chumba cha upasuaji, mara baada ya kufanyiwa upasuaji walikuja kukabidhiwa mgonjwa aliyefanyiwa upasuaji wa kichwa lakini hakuwa ndugu yao.
�Tulipokabidhiwa na wauguzi tulimkataa kwa kuwa hakuwa ndugu yetu na hapo ndipo tulipoanza kumtafuta ndugu yetu, katika kumtafuta tulimkuta amefanyiwa upasuaji wa mguu na si kichwa kama ilivyokuwa inatakiwa,�anasema Mgina.
Naye Sisti Marishay ambaye ni kaka wa Emmanuel Didas ambaye amefanyiwa upasuaji wa kichwa badala ya mguu anasema Didas alifikishwa hospitalini hapo kutokana na kuumia goti baada ya kupata ajali ya pikipiki hivi karibuni na kisha kulazwa katika Taasisi ya Mifupa (MOI).
Marishay anasema ndugu yake Didas akiwa hospitalini hapo alipigwa picha za x-ray ambazo zilionyesha kuwa hakuwa na matatizo katika mifupa ila alikuwa na uvimbe kwa ndani ndipo madaktari wakashauri afanyiwe upasuaji ili kuondoa uvimbe huo.
Lakini katika hali ya kusikitisha madaktari wakamfanyia upasuaji wa kichwa, wakati hakuwa na tatizo lolote la kichwa, anasema Marishay.
�Naweza kusema kuwa kilichofanyika ni uzembe wa hali ya juu, mdogo wangu alikuwa haumwi kichwa lakini nashangaa amefanyiwa upasuaji wa kichwa na baada ya kutokea tatizo hilo nimezungumza na Mkurugenzi Mkuu wa Taasisi hiyo Profesa Laurent Museru ambaye alikiri kuwa kuna makosa yametokea hivyo wameamua kukaa na kuunda tume ya kuchunguza uzembe huo, kisha tume hiyo itatoa taarifa baada ya wiki moja,� anasema Marishay.
Wakati huo huo ndugu mwingine Ludani Didas anasema kwa sasa hawezi kuzungumza chochote kwa kuwa mpaka sasa mdogo wake hajitambui, hawezi kuzungumza chochote na yuko ICU, �ni vyema tukasubiri tuone hatima ya Afya yake ndipo nitakapoweza kuzungumzia uzembe huu wa wazi tena wanaofanyiwa wanyonge.�
Baadhi ya wananchi waliozungumzia tukio hilo walisema kwamba tukio hilo linasikitisha na ni vigumu kuelezewa kwa sababu mazingira yaliyo sababisha upasuaji tata huo hayajajulikana japo kuwa inaweza kutafsiriwa kama uzembe wa Wauguzi, Madaktari na idara nzima ya huduma katika taasisi hiyo.
Licha ya jamii kusikitishwa na tukio hilo, wapo pia madaktari bingwa wa upasuaji ambao wameonekana kushangazwa Kutokana na tukio hilo kwa kuwa kabla ya upasuaji wowote kufanyika zipo hatua sita ambazo zinatakiwa kupitiwa na wataalam saba wa afya kabla ya upasuaji.
Madaktari hao wameelezea hatua hizo kuwa ni mgonjwa kupigwa picha ya x-ray kabla ya upasuaji wowote ili kubaini tatizo linalo msumbua baada ya hatua hiyo kuna daktari atakaye husika na upasuaji huo anatakiwa kuisoma x-ray hiyo na kumtambua mgonjwa wake.
Hatua ya pili ni msimamizi wa zamu wodini anatakiwa kuwasiliana kwa karibu na daktari ili kufahamu siku maalum ya kumfanyia mgonjwa huyo upasuaji sanjari na kuwataarifu ndugu wa mgonjwa husika.
Wataalam hao wameongeza kwamba hatua ya tatu ni kumuandaa mgonjwa kwa kumueleza hali halisi ikiwa ni pamoja na kuandaa mahali ambapo anatakiwa kufanyiwa upasuaji huo kama ni kichwani anatakiwa kunyolewa nywele na kufungwa plasta mahali husika.
Hatua ya nne daktari anatakiwa kumuona mgonjwa siku moja ama mbili kabla ya siku ya kufanyiwa upasuaji hatua ya tano ni mgonjwa kutolewa wodini kwenda katika chumba cha upasuaji akiwa na wauguzi wawili na jalada lake kadhalika msimamizi wa zamu wodini na wauguzi hao wawe wamesaini katika faili la mgonjwa.
Wakizungumzia hatua hizo madaktari hao wamesema kwamba hatua ya sita ambayo ni ya msingi zaidi ni wakati wauguzi wa wodini wanapokabidhiwa mgonjwa, kabla ya kumpokea wanapaswa kumkagua kwanza kama ameambatana na vibali vyake vyote na kumtambua kwa kumuita majina yake mawili kama ni mgonjwa anayeweza kuzungumza.
Wamefafanua kwamba kama hawezi kuzungumza wanapaswa kuwauliza ndugu wa mgonjwa kwa sababu wanapaswa kuwepo kwani ni makosa kumuondoa mgonjwa wodini na kumpeleka katika chumba cha upasuaji bila ndugu zake kufahamu wala kuwapo.
Baada ya hatua hiyo wauguzi hao wanapaswa kusaini kabla ya kumuingiza mgonjwa katika chumba hicho hata hivyo wamesema kwamba mgonjwa akisha ingizwa katika chumba cha upasuaji daktari wa usingizi anapaswa kumkagua mgonjwa na kuzungumza naye ama kuzungumza na ndugu zake ili ahakikishe kwamba huyo ndiye.
Ndipo daktari wa upasuaji anamkagua na kuzungumza naye kwa mara nyingine huku akimuondolewa wasiwasi ili mgonjwa aweze kumzoea na hata atakapo zinduka baada ya upasuaji awe anauwezo wa kukumbuka mambo aliyozungumza mara ya mwisho kabla ya kuchomwa sindano ya usingizi sanjari na kumkumbuka daktari wake.
Wameeleza kwamba baada ya hapo ndipo mgonjwa huyo anapaswa kuchomwa sindano ya usingizi (nusu kaputi) kisha ndipo daktari aanze kazi ya kumpasua mgonjwa huyo. Wanasema kuwa kwa kupitia hatua zote hizo si rahisi makosa kama hayo kutokea japokuwa ni makosa ya kibinadamu lakini pia wanapaswa kuzingatia kanuni zote hizo ili kuepukana na makosa kama hayo.
Madaktari hao wameeleza kwamba hilo si tukio la kwanza kutokea katika taaluma yao, ila huenda likawa ni la kwanza masikioni mwa Watanzania hivyo limeweza kusababisha mfadhaiko hususan kwa wale waliopatwa na tukio hilo.
Wamesema kwamba kila daktari anapenda mgonjwa wake apone na inapotokea vinginevyo huwa wanakosa raha, wakati mwingine wanarudi nyumbani wakisikitika huku wakipekua upya kurasa za vitabu ili wafahamu sababu zaidi inayomfanya mgonjwa asipone.
�Sasa kutokana na kanuni na baadhi ya taratibu hizo, daktari hawezi kufanya kosa kubwa kama hilo, sisi tuna wasiwasi kwa nini tukio kubwa kama hilo limetokea kama kweli wataalamu wote walifuata kanuni hizo, wanasema madaktari hao bingwa�.
Pia kuna kanuni zilizowekwa kitaalamu kabla ya kumfanyia upasuaji mgonjwa, lakini siku hizi watu wamezoa kufuata njia za mkato badala ya kufuata kanuni na taratibu zilizowekwa kitaalamu kwa ajili ya upasuaji.
Na kuwa linapotokea tatizo kwa upande wa afya kuna njia tatu ambazo wasimamizi wa vitendo wametakiwa kuzifuata kabla ya kuchukua hatua yoyote.
�Linapotokea tatizo la afya kuna njia tatu ambazo wasimamizi wa vitengo wanatakiwa kuzifuata kabla ya kuchukua hatua yoyote ikiwa ni pamoja na kutoa taarifa Wizarani, kuwasilisha taarifa baada ya kufanya uchunguzi wa tatizo hilo na kisha Baraza la Madaktari linapaswa kuketi kwa ajili ya kujadili na kutoa taarifa yake,� wanasema madaktari hao.
Kwa mujibu wa uchunguzi uliofanywa na gazeti hili, Novemba 8 ilibainika kuwa, Daktari aliyepangwa kupasua hakutokea, alikuwa na udhuru. Pia mgonjwa aliyetakiwa kufanyiwa upasuaji wa kichwa hakuwa amenyolewa nywele na badala yake, wauguzi walifanya kazi hiyo baada ya kuulizwa.
Vilevile ilibainika kuwa, Daktari aliyesimamishwa kazi baada ya kufanya upasuaji tata huo siku ya tukio hakuwa zamu ila alifika hospitalini hapo kwa lengo la kumzibia pengo daktari aliyetakiwa kufanya upasuaji.
Uchunguzi huo pia ulibaini kuwa, Daktari huyo hakuwahi kumuona mgonjwa kabla ya kumfanyia upasuaji na kwamba alipoingia kwenye chumba cha upasuaji, alikuta mgonjwa ameshapigwa sindano ya nusu kaputi.
Mara baada ya Daktari huyo kukamilisha upasuaji huo alimkabidhi mgonjwa kwa wauguzi ili wamrudishe wodini.
Sasa kutokana na kusimamishwa kwa daktari huyo ambaye ndiye bingwa wa upasuaji wa kichwa kumekuwapo na msongamano mkubwa wa wagonjwa kwa kuwa yeye ndiye aliyekuwa msimamizi wa madaktari wengine wakati wa upasuaji.
Kutokana na tukio hilo, mnamo Novemba 6, Mkurugenzi wa Hospitali hiyo Profesa Laurent Museru aliagiza kuundwa kwa tume ili kuchunguza kwa undani tukio la wagonjwa hao.
Tume hiyo ambayo ina wajumbe sita, inaongozwa na Profesa Victor Mwafongo wa Hospitali ya Taifa Muhimbili.
Kuwapo kwa tume hiyo itasaidia Serikali kuchukua hatua zinazotakiwa endapo watu watabainika kutenda kosa ama kufanya uzembe uliosababisha kosa kutendeka.
Akizungumza ofisini kwake Mganga Mkuu wa Serikali, Deo Mtasiwa alisema, Serikali haiwezi kupuuza tukio hilo, lakini inahitaji kupata taarifa za kweli.
�Tunaitaka tume ifanye kazi hiyo haraka, kisha kuleta majibu ili tuweze kutoa tamko mara moja,� alisema Dk. Mtasiwa.
Naye, Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Profesa David Mwakyusa amesema amewataka wananchi wasubiri taarifa kamili itakayotolewa na tume na kisha kutoa rai kwa vyombo vya habari huku akisisitiza kuwa jambo hili ni zito hivyo ni vyema lizungumzwe kwa undani.
Mwakyusa anasema upotoshaji unaweza kuleta hofu isiyo ya kawaida kwa wananchi.

Sunday, November 25, 2007

Kina Mama wapo mbele katika ujenzi wa Taifa

Hapa Wamama hawa wawili niliwakuta sehemu ya Kariakoo wakichanganya zege
katka kutafuta maisha.

hapa kazi inaendelea kama kawa kwenye kazi hiyo bila kujali jinsia, ndio maisha yanapoendelea

DSM INAPENDEZA LAKINI!

DSM inabadilika siku hizi Mambo safi lakini sio sana
Hapa kama unaelekea Kigamboni utakutana na miundombinu hiii

Kazi inawezekana pia









  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.comme google-site-verification=Qm-XNfnL5kai8WV2inT1RRX2WIPaBTG_WPq3kYSBwbgKennedy Kimaro 2008 NYUMBANI NI NYUMBANI TU KUMBUKA KUWEKEZA NYUMBANI LEO

Rudi TOP-Juu