Tuesday, November 20, 2007

Kamati Kuu Chadema kujadili uteuzi wa Zitto














Kamati Kuu Chadema kujadili uteuzi wa Zitto

*Mbowe akatisha masomo kuhudhuria kikao


*Mtei asema maslahi ya taifa hayana chama


*Zitto asema hajitoi labda Rais amfukuze


*Mnyika: Mkono wa CCM umepenyezwa


Waandishi Wetu
KAMATI Kuu ya Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) inakutana Jumamosi wiki hii kujadili pamoja na mambo mengine uteuzi wa Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe kwenye Kamati ya kupitia upya mikataba ya madini nchini.
Zitto ni miongoni mwa wajumbe 11 walioteuliwa na Rais Jakaya Kikwete kwa ajili ya kupitia upya mikataba ya madini na Sheria za Madini kwa lengo la kuwanufaisha Watanzania.
Habari kutoka ndani ya Chadema zinasema kwamba kutokana na mjadala wa uteuzi wa Zitto kuibuka ndani ya chama hicho, Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe kwa kushirikiana na viongozi wa juu ameitisha Kamati Kuu ya dharura kujadili hali hiyo. Kwa sasa Mbowe yuko masomoni nchini Uingereza.
"Hali imekuwa ngumu, inaonekana kuna watu wameingiza mkono katika huu uteuzi wa Zitto, hivyo chama kimeamua kuitisha Kamati Kuu ya dharura kujadili suala hili. Kikao kitafanyika Jumamosi jijini Dar es Salaam," alisema kiongozi mmoja katika Makao Makuu ya chama hicho ambaye hakutaka kutaja jina lake.
Mwananchi iliwasiliana na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa kujua ukweli wa kuwepo kwa mkutano wa Kamati Kuu, ambaye akiri na kusema kuwa wameamua (viongozi) kuitisha mkutano wa dharura kutokana na kujitokeza kwa kauli tofauti kutoka kwa baadhi ya wananchama na viongozi kuhusiana na uteuzi huo wa Zitto kwenye kamati ya madini .
"Ni kweli tumeamua kuitisha Kikao cha Kamati Kuu ambacho kina maamuzi katika chama, ili kujadili kauli hizo za viongozi wa chama ambazo zimejitokeza sasa. Chadema haizui watu kuwa na mawazo tofauti, lakini lengo la kikao cha Jumamosi ni kutoa tamko la chama kuhusiana na suala hilo," alisema.
Alisema katika kikao cha Jumamosi, Chadema itatoa msimamo wa chama kuhusiana na Kamati ya Madini iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete na uteuzi wa Zitto katika Kamati hiyo ya kupitia mikataba ya madini.
Wakati Kamati Kuu ya Chadema ikipanga kukutana, Zitto amesema hawezi kujitoa katika kamati hiyo kama baadhi ya watu wanavyoshauri kwa kuwa suala la kupitia upya mikataba hiyo, limo katika sera za Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) ambayo yeye ni mwanachama wake.
Sera ya Chadema ya madini, pamoja na mambo mengine, inaeleza kuwa: "Mikataba yote ya uchimbaji madini, itapitiwa upya na kuwekwa wazi kwa wananchi na kwamba kuanzia asilimia thelathini ya mapato yatokanayo na madini yatabaki nchini".
Akizungumza na Mwananchi jana, Zitto ambaye pia ni Naibu Katibu Mkuu wa Chadema alisema kutokana na sera hiyo ya chama chake, anaamini kuwa madini ni moja ya rasilimali zinazowanufaisha Watanzania kiuchumi kwa hiyo amejiandaa vema kutekeleza majukumu yake kwenye kamati kwa niaba ya chama chake na Watanzania, hivyo hawezi kujitoa kwenye kamati hiyo, labda Rais Kikwete amfukuze.
"Sitajitoa kwenye kamati, kwa kuwa kupitia mikataba ya madini ni sera ya Chadema, CCM (Chama Cha Mapinduzi) hawana sera ya aina hii. Hivyo, nitaendelea kushikilia msimamo huo labda rais anifukuze," alisema Zitto.
Alisema hayuko tayari kuipoteza fursa aliyoipata kwa kuwa hafahamu namna wananchi watakavyopokea iwapo ataamua kujitoa katika kamati hiyo, kama baadhi ya watu wanavyoshauri.
Akitoa maoni yake Muasisi wa Chadema, Edwin Mtei alisema anaunga mkono uteuzi wa Zitto katika kamati hiyo kwa kuwa ana sifa na pia tatizo la madini linapaswa kushughulikiwa na kila Mtanzania.
"Hata Chadema walimteua Zitto kuwa Naibu Katibu Mkuu kwa sababu ya misimamo yake na pia inapofika suala la madini, Mtanzania yeyote anatakiwa kuchangia," alisema Mtei.
Hata hivyo, Mtei alisema watu kuwa na mitazamo tofauti katika mambo ni jambo la kawaida, lakini linapojitokeza suala linalogusa maslahi ya taifa, wazalendo wa kweli wanatakiwa kuunga mkono na si kupinga.
"Watu wote wanatakiwa waunge mkono, sababu suala la madini ni rasilimali za nchi ambayo inawanufaisha Watanzania. Kazi ya upinzani si kupinga tu. Hivyo, sioni sababu yoyote ya Zitto kujitoa kwenye kamati," alisema Mtei.
Naye Mkurugenzi wa Vijana wa Chadema, John Mnyika alisema ana mashaka kwamba baadhi ya watu kutoka CCM wameshaanza kutumia hali ya sasa ya viongozi kuwa na kauli za kutofautiana kufanya propaganda kuwa kuna mgogoro ndani ya Chadema na
kwamba chama hicho kinatanguliza maslahi ya kisiasa ya upinzani badala ya maslahi ya Taifa.
Wakati huo huo, UMOJA wa Vijana wa CCM umesema kuwa umeshangazwa na kauli iliyotolewa na Katibu Mkuu wa Chadema Dk Wilibroad Slaa kuwa chama hicho hakina imani na kamati ya kupitia upya mikataba ya madini iliyoteuliwa na Rais Kikwete hivi karibuni.
Akitoa taarifa jana Kaimu Katibu Mkuu wa Umoja huo Amos Makalla, alisema kauli hiyo inashangaza na akamtaka kiongozi huyo atulie na aiachie kamati hiyo ifanye kazi zake kwa uhuru.
Hata hivyo, wakati Zitto na Mtei wakisema hayo, Kaimu Katibu Mkuu wa Chadema, Victor Kimesera alisema jana kuwa chama chake kinaitaka serikali iwe imezipatia ufumbuzi hoja za chama hicho za kupinga kuundwa kwa kamati hiyo ifikapo Novemba 25, mwaka huu.
Kimesera ambaye alizungumza na Mwananchi ofisini kwake jijini Dar es Salaam jana alisema, Chadema inapinga kamati hiyo kwa kuwa wajumbe wake wengi wanatoka kwenye chama kimoja (CCM).
Alisema hali hiyo inainyima kamati hiyo uhalali wa kisheria kudai nyaraka au chochote kwa ajili ya kutekeleza majukumu yake.
"Bunge ndilo lililopaswa kuunda kamati hiyo kwa kuwa ingepata nguvu ya kisheria. Hizo ni' blabla' tu na Zitto atajikuta ameingizwa kwenye kitu ambacho hakitazaa matunda," alisema Kimesera.
Hata hivyo, alisema tangu kuundwa kwa kamati hiyo, hakuna lolote lililobadilika katika chama na kwamba, umoja na mshikamano ndani ya chama bado upo kinyume na inavyotangazwa na baadhi ya watu.
Alisema wanachokikataa wao na ambacho kinaonekana kuwa ni mgogoro ni chama kuendeshwa na fikra za mtu mmoja.
"Kila mtu afikiri anavyoona na ni haki yake, lakini tunachokikataa ni ile dhana ya 'zidumu fikra za mtu mmoja'," alisema Kimesera.
Kamati hiyo yenye wajumbe 11, iliundwa na Rais Jakaya Kikwete wiki iliyopita na iko chini ya uenyekiti wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali Mstaafu, Jaji Mark Bomani.
Tangu Rais Kikwete aunde kamati hiyo na kumteua Zitto kuwa mmoja wa wajumbe wake (kamati hiyo), baadhi ya watu, wakiwamo wafuasi wa chama hicho wakiongozwa na Mbunge wa Tarime (Chadema), Chacha Wangwe, wamekuwa wakipinga uteuzi huo wa Zitto kwa madai kwamba, unadhoofisha hoja za wapinzani na kujenga usaliti baina yao kuhusiana na suala la madini nchini.
Novemba 13, Mwaka huu Rais Kikwete alitangaza kuundwa kwa Kamati ya kupitia mikataba na sheria za madini na kuwateua wajumbe wa kamati hiyo iliyojumuisha wajumbe kutoka kambi ya upinzani akiwemo Zitto wa Chadema.
Mbali na Zitto, wengine wanaunda Kamati hiyo, ni Mbunge wa Bariadi Mashariki (UDP), John Cheyo, Mwanasheria wa Wizara ya Nishati na Madini, Salome Makange, Kamishina wa Sera Wizara ya Fedha, Mugisha Kamugisha, Mkurugenzi Msaidizi Idara ya Makazi Wizara ya Ardhi, Edward Kihundwa na Mbunge wa Kyela (CCM), Dk. Harrison Mwakyembe.
Wajumbe wengine, ni Mbunge wa Msalala (CCM), Ezekiel Maige, Peter Machunde kutoka Soko la Hisa, Dar es Salaam (DSE), Mkaguzi wa Mahesabu kutoka Kampuni ya Kimataifa ya Ukaguzi wa Mahesabu, Price Water Coopers, David Tarimo ambaye ni mtaalamu wa masuala ya kodi na Mkurugenzi wa Madai na Sheria za Kimataifa, Wizara ya Katiba na Sheria, Maria Kejo.
Imeandaliwa na Muhibu Said, Elizabeth Suleyman na Salim Said wa MUM

  © Blogger templates 'Neuronic' by Ourblogtemplates.comme google-site-verification=Qm-XNfnL5kai8WV2inT1RRX2WIPaBTG_WPq3kYSBwbgKennedy Kimaro 2008 NYUMBANI NI NYUMBANI TU KUMBUKA KUWEKEZA NYUMBANI LEO

Rudi TOP-Juu